Tuesday 28 March 2017

Jinsi Perisic anavyoweza kufiti Man Utd na kuwateka mashabiki


Staa Ivan Perisic ni mmoja kati ya wachezaji wenye vipaji vya hali ya juu wanaohusishwa kujiunga na Manchester United wakati wa usajili wa majira haya ya joto.

Kwa sasa mashetani hao wekundu wanatajwa kuwa ndio wanaoongoza katika mbio za kuwania saini ya straika huyo wa Inter Milan, baada ya kocha wao, Jose Mourinho, kunaswa akimshuhudia wakati wa mchezo ambao  Croatia waliibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Ukraine katika mechi za kufuzu fainali za Kombe la Dunia.

Lakini Mreno huyo anakana taarifa hizo akisema kuwa hakwenda kumfuatilia staa huyo, huku akidai kuwa ukweli ni kwamba alikwenda nchini humo kwa ajili ya kukimbia hali ya hewa ya mvua inayoendelea kunyesha katika jiji la Manchester.

Hata hivyo, pamoja na Mourinho kumkana raia huyo wa Croatia, wapo wengi ambao wanaamini kuwa staa huyo anaweza kuwa msaada mkubwa kwa mashetani hao wekundu na huku zikitajwa sababu za kumfanya awe kivutio kwa mashabiki endapo atajiunga na klabu hiyo ya Old Trafford.

Moja ya sababu zinazotajwa ni kwamba, hakuna siri mashabiki wa  Man United kwa sasa wanatarajia kushuhudia soka la kuvutia, kushambulia na Perisic anaonekana kuwa anaweza kulileta kwenye klabu hiyo ya Old Trafford kutokana na uchezaji wake.

Inaelezwa kuwa kama ilivyo kwa Zlatan Ibrahimovic, ambaye ameng’ara tangu aliposajiliwa na Man United akiwa mchezaji huru mwanzoni mwa msimu huu, kinara huyo raia wa Croatia mara zote huwa anapenda kufunga kwa staili ya kuvutia.

Jambo hilo amekuwa akilidhihirisha hata akiwa mazoezini ama mbele ya maelfu ya mashabiki uwanjani ambapo Perisic amekuwa akionesha umahiri wake wa kucheka na nyavu kwa staili ya aina yake.

Mbali na hilo, staa huyo mwenye umri wa miaka 28, si mwoga kutunisha misuli yake na amekuwa akijituma zaidi akiwa katika mazoezi ya gym. Pia  nguvu zake kimwili na uwezo wake wa kukimbia vinamjenga kuwa na uwezo wa kucheza kwenye michuano ya Ligi Kuu England kutokana na kwamba anaweza kukabiliana na mabeki visiki.

Endapo Antonio Valencia, ambaye  Mourinho mara zote amekuwa akimwita kuwa ndiye beki bora wa kulia duniani tayari atakuwa amepata rafiki kutokana na kuwa na yeye pia ni kipenzi cha kujifua gym. Pia staa huyo wa timu ya Taifa ya  Croatia anatajwa kuwa na kitu ambacho anacho staa mwingine wa Man United, Paul Pogba.

Inaelezwa kuwa kama ilivyo kwa staa huyo ambaye alisajiliwa kwa usajili uliovunja rekodi, Perisic anafurahi kutengeneza nywele na mara zote amekuwa akishuhudiwa kunyoa kiduku kama alivyo Mfaransa huyu ambaye alisajiliwa kwa pauni milioni 90.

No comments:

Post a Comment