Saturday 9 January 2021

Mastaa hawa wana dalili za kuaga ukapera 2021

 Mwaka jana zaidi ya mastaa nane walifunga ndoa. Mwaka huu ni kina nani wataingia kwenye safina hiyo ngumu kuchonga? hapa nakupa uchambuzi wa mastaa wenye dalili ya kufunga ndoa mwaka 2021 ikiwa ni pamoja na asilima za uwezekano wa kuwepo kwa ndoa hizo kwa kila msanii husika.

SHILOLE 95%

Shishi Biden alimaliza mwaka 2020 akiwa na pete ya uchumba kidoleni aliyovalishwa na bebi wake mpya, mpiga picha anayefahamika kwa jina la Rommy 3D.

Kwanini tunadhani Shilole ana 95% ya kufunga ndoa mwaka huu? Ni kwa sababu kwanza ana pete ya uchumba tayari, pili Shilole mwenyewe anakiri kuwa kwa hatua aliyofikia sasa hawezi kuwa na mpenzi tu bila ndoa, ana watoto wakubwa, ana majukumu makubwa, hawezi kuvumilia mapenzi ya ujana ujana kwahiyo kwake ndoa ni kitu muhimu kama kitambulisho ya Nida.

Tatu, Shishi Baby na mpenzi wake wa sasa wana historia kubwa sana ya mapenzi, ambayo walisimulia wenyewe kupitia Instagram zao kwamba walikuwa wapenzi zamani na mipango yao ilikuwa ni kuoana lakini waliachana kutokana na sababu za kimaisha, sio kwamba waligombana au walitengana kwa shari. Na kwa sasa wako pamoja na kwa kuwa hizo sababu za kimaisha hazipo tena, kwahiyo ni kitu gani kinaweza kuwazuia wasifunge ndoa mwaka huu?

Nne ni hata ukipita Instagram zao, utagundua kuwa mahaba yao ni ya moto kweli kweli. Mmoja asipokula mwingine chakula hakishuki kooni. Na hivi tunavyozungumza Shilole amempeleka mumewe mtarajiwa kwao Igunga kwa ajili ya kumtambulisha kwa wakwe na mashemeji.

Pia Shilole anaweza kuamua kuolewa ili amuumize moyo mumewe wa zamani Uchebe ambaye mpaka sasa bado wanapigana vijembe huko mitandaoni. Sio sababu nzito lakini ni nani anayeweza kuelewa akili za wasanii zinavyofanya kazi? Ziko tofauti sana.

VANESSA MDEE 80%

Masaa machache kabla ya kuingia mwaka mpya 2021 Vanessa Mdee alipewa zaidi ya kuvalishwa pete ya uchumba na mpenzi wake, muigizaji wa Marekani mwenye asili ya Nigeria, Olurotimi Akinosho ‘Rotimi’.

Tunadhani Vee Money ana asilima 80 ya kufunga ndoa mwaka huu na Rotimi wake kwa sababu tayari ana pete uchumba. Pili yeye na Baby wake mapenzi yao yamenoga kama ya Adamu na hawa uko Instagram. Ukiingia tu unakutana na picha, wamepostiana, hujakaa vizuri hao wapo wanafanya video live, ni shida.

Tatu Rotimi mwenyewe anadai Vanessa ni mtu sahihi zaidi kuwa mke wake kwa sababu alikaa naye ndani kipindi nchi ya Marekani ipo kwenye ‘lockdown’ ya corona, kwahiyo anaamani kama aliweza kufurahia naye maisha wakiwa wawili tu bila kuboreka, maana huyo ni mtu sahihi kwa ajili ya maisha yake yote.

Na nne, wakati anafanya Instalive hivi majuzi Januari 4, shabiki mmoja alimuuliza kuhusu mipango yao ya kufunga ndoa, Vanessa alijbu itafanyika hivi karibuni.

Kama hiyo haitoshi, aliulizwa kuhusu mtoto, akasema wanatazamia kupata mtoto kabla ya mwaka huu kuisha. Hii ni sawa na kusema utajuaje kama wamepanga kupata mtoto wakiwa tayari kwenye ndoa? Kwahiyo kama mtoto atapatikana mwaka huu kuna uwezekano mkubwa ndoa ikawa mwaka huu pia.

BILLNAS & NANDY 70%

Kila mtu anajua kuwa tayari Billnas alishamvisha pete Nandy. Pete ambayo baadae familia ya Nandy ilikataa kuitambua kwa sababu haikufuata taratibu; waliwalishana jukwaani.

Hata hivyo Billnas akaona isiwe poa, akatuma wazee waende kwa kina Nandy kujitambulisha na wakafanya hivyo. Na kwa mujibu wa Nandy mwenyewe aliandika kwenye Instagram yake kuwa barua ya Billnas iimepokelewa na kupata majibu mazuri.

Kinachofuata baada ya hapo ni ndoa tu na ndiyo maana tunasema kuna 70% za ndoa hiyo ikafanyika mwaka huu 2021.

ELIZABETH MICHAEL 55%

Aisee! Elizabeth Michael ‘Lulu’ anatembea na pete ya uchumba aliyovishwa na Majizo kwa zaidi ya miaka miwili sasa mpaka mashabiki zake wamechoka kiasi kwamba akipost chochote kwenye Instagram yake watu huandika kumuuliza kuhusu anaolewa lini.

Unaambiwa mpaka aliyekuwa mkuu wa mkoa wa Dar es salaam, Paul Makonda alikuwa muangalizi wa uhusiano huu kuanzia mwaka 2018 lakini mwaka ukapita bila ndoa, 2019 ikapita na 2020 pia ikapita bila mchumba wa Lulu ambaye ni mmiliki wa EFM na ETV kufunga ndoa na mdogo wetu.

Pia inadaiwa Oktoba mwaka jana ndoa ya wiwili hao ilitangazwa Kanisa Katoliki la Mtakatifu Andrea Bahari Beach jijini Dar es Salaam. Hilo lilikuwa tangazo la kwanza na kwamba, baada ya wiki mbili mbele ilitakiwa wawili hao waunganishe miili kuwa kitu kimoja, lakini mwaka uliisha bila hilo kuwekezekana.

Sasa kwa sababu haifahamiki wazi wazi ni nini haswa kilikwamisha washindwe kufunga ndoa mwaka jana, bila shaka kuna nafasi kubwa ya wao kufikia utatuzi na ndoa ikawezekana mwaka huu.

DIAMOND 51%

Mwaka jana ilibaki kidogo tu Diamond amuoe mama wa mtoto wake wa mwisho, muimbaji kutoka Kenya, Tanasha Dona. Kulikuwa na viashiri vyote lakini hata yeye mwenyewe aliwahi kuzungumzia utayari wake katika hilo. Lakini sijui Tanasha alimchokoza nini kaka yetu, wakatemana na mipango ya ndoa ikafia huko.

Na ndani ya mwaka 2020 karibu kila mtu wa karibu wa Diamond alikuwa akimsukuma kuoa. Meneja wake walikuwa wakimpiga vijembe aoe, dada zake Esma na Queen Darleen, hata mama yake na baba zake wote wawili, ,mzazi na wa kufiki wanaonesha kutumani kuona mtoto wao akioa kwa mwaka jana. Hata hivyo kwa sababu hilo lilishindakana 2020, kabda litawezekana mwaka huu; hata hivyo jamaa haeleweki kwenye mambo ya mahusiano ndiyo maana ndoa yake inatazamiwa kwa asilimia 51 tu.



No comments:

Post a Comment